Raia 4 wa Burundi wakamatwa Kenya wakienda kujiunga na Al Shabab
Raia wanne wa Burundi wamekamatwa katika eneo la Merire katika barabara Kuu ya kutoka Isiolo kwenda mjini Marsabit.
Imechapishwa:
Maafisa wa usalama wanasema raia hao wa kigeni walikuwa njiani kwenda nchini Somalia kujiunga na kundi la kigaidi la Al Shabab.
Aidha, imebainika kuwa watu hao walikuwa wameingia nchini Kenya wakitokea jijini Bujumbura kama watalii wa kawaida.
Raia hao waliokamatwa ni pamoja na Ntakarutimana Benerd, 41, Niyongere Yusuf, 32, Nshimirimana Fulgnce Shadady, 31 na Bizoza Abderauf, 20.
Watu hao walikamatwa mapema siku ya Jumanne mwendo wa saa 10 Alfajiri na wanachunguzwa zaidi kuhusu uhusiano wao na Al Shabab.
Mwezi Juni, Wakenya watano walikamatwa katika eneo hilo nao wakienda nchini Somalia kuungana na kundi hilo la kigaidi.
Idadi kubwa ya vijana wanaoishi Pwani ya Kenya, na hasa Kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo wanaaminiwa kuwa wamekwenda kujiunga na kundi hilo.
Chanzo kubwa cha vijana wengi kuungana na kundi hili kinaelezwa kuwa ni ukosefu wa ajira.
Wakati uo huo, maafisa wa usalama wameendelea kukabiliana na washukiwa wa Al Shabab katika msitu wa Boni katika Kaunti ya Lamu.
Siku ya Jumatatu, watu 12 walipoteza maisha kuvamia makaazi ya watu katika mji wa Bulo Hawo karibu na mji wa Mandera unaopakana na nchi ya Somalia.