Nchi za NATO zakubali kutuma mifumo zaidi ya ulinzi wa anga kwa Kyiv
Nchi za NATO zimekubali kuitumia Ukraine mifumo zaidi ya ulinzi wa anga, zikiwemo betri za Patriot, Katibu Mkuu wa NATO Jens Stoltenberg ametangaza siku ya Ijumaa.
Imechapishwa:
"NATO imekagua uwezo uliopo ndani ya Muungano na kuna mifumo ambayo inaweza kupatikana kwa Ukraine. Kwa hiyo ninatarajia matangazo mapya kuhusu mifumo ya ulinzi wa anga hivi karibuni,” amesema Jens Stoltenberg, kufuatia mkutano kati ya mawaziri wa ulinzi wa NATO na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky, ambao unafanyika kwa njia ya video.
Hayo yanajiri wakati wanachama wa G7 wameahidi kuendelea kuisaidia Ukraine katika ulinzi wa angani.
Mawaziri wa mambo ya kigeni wa nchi za G7, ambao wamekutana katika kisiwa cha Capri nchini Italia, wameahidi kuendelea kuisaidia nchi ya Ukraine kuimarisha ulinzi wake wa agani.
Katika taarifa yao, mawaziri hao wameeleza kuwa wanatafuta namna ya kuzitumia mali za Urusi ambazo zimezuiliwa kuisaidia Kyiv.
Viongozi hao wamekutana kuelekea kikao cha wakuu wa nchi za G7 mwezi Juni mwaka huu.
Ukraine imesema inakaribia kuishiwa na silaha za kudungua makombora ya Urusi na ndege zisizo na rubani, hatua inayokuja wakati huu ambapo Urusi imeonekana kuimarisha mashambulio dhidi ya miundombinu ya Kyiv.
Tayari waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani David Cameron alikuwa amewashinikiza washirika wa G7 kutafuta namna ya kutumia mali za Urusi zilizozuiliwa baada yake kuivamia Ukraine mwaka wa 2022 kuisaidia Kyiv.