Uturuki: Mmoja afariki na kumi na wawili kujeruhiwa kando ya uchaguzi wa serikali za mitaa
Angalau mtu mmoja ameuawa na watu wengine kumi na wawili wamejeruhiwa Jumapili Machi 31 nchini Uturuki wakati wa matukio ya kando ya uchaguzi wa serikali za mitaa huko Diyarbakir, jiji kuu la Wakurdi (kusini-mashariki), imetangaza Wizara ya Afya.
Imechapishwa:
"Mapigano yalizuka kati ya makundi mawili wakati wa uchaguzi siku ya Jumapili na kusababisha mtu mmoja kufariki na kumi na wawili kujeruhiwa," afisa mmoja pia ameliambia shirika la habari la AFP, akibainisha kuwa matukio haya yalitokea katika kijiji kilichoko kilomita 30 kutoka mji mkuu wa mkoa.
Waturuki wamepiga kura Jumapili katika uchaguzi wa serikali za mitaa unaolenga jitihada za Rais Recep Tayyip Erdogan kuchukua tena udhibiti wa Istanbul kutoka kwa mpinzani Ekrem Imamoglu.
Meya wa Istanbul Imamoglu alimpa Erdogan na chama chake cha AK kipigo kikubwa kuwahi kushuhudiwa katika miongo miwili madarakani kufuatia ushindi wake katika uchaguzi wa 2019. Rais huyo alirejea tena mwaka wa 2023 kwa kuchaguliwa tena na wingi wa viti bungeni na washirika wake wa siasa kali za kizalendo.
Matokeo ya leo huenda yakaimarisha udhibiti wa Erdogan kwa Uturuki ambayo ni mwanachama huyo wa Jumuiya ya Kujihami NATO, au kuashiria mabadiliko katika mazingira yaliyogawanyika katika dola hilo kubwa linaloibukia kiuchumi. Ushindi wa Imamoglu unaonekana kuchochea matarajio ya yeye kuwa kiongozi wa siku zijazo wa kitaifa.