G7 yatoa wito kwa wafadhili wa Ukraine kuidhinisha misaada yao ya kifedha kwa 2024
Kundi la mataifa 7 yaliyostawi zaidi kiviwanda, G7, limetoa wito kwa wafadhili wa Ukraine kuidhinisha mchango wao wa kifedha kwa mwaka 2024, bila hata hivyo kutaja moja kwa moja kuzuiwa kwa msaada mpya wa Marekani kwa Congress.
Imechapishwa:
"Tunaomba kuidhinishwa kwa msaada wa ziada ili kukidhi mahitaji ya bajeti iliyobaki ya Ukraine mwaka 2024," wamesema viongozi wa G7 (Marekani, Japan, Ujerumani, Ufaransa, Uingereza, Italia, Canada) katika taarifa ya pamoja kwa vyombo vya habari baada ya mkutano wa kilele kwa njia ya video chini ya uongozi wa Italia.
G7 pia imelenga China na Iran kwa msaada wao wa vifaa kwa Urusi katika vita vyake dhidi ya Ukraine, ikitoa wito kwa Tehran "kusimamisha" misaada yake na kuelezea wasiwasi kwamba makampuni ya China yanaipatia Moscow vifaa vya kijeshi.
"Tunatoa wito kwa Iran kuacha kusaidia jeshi la Urusi," wamesema viongozi wa G7 ambapo Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron, hakuwepo, nafasi yake ilichukuliwa na Waziri wake wa Mambo ya Nje Stéphane Séjourné.
Korea Kaskazini pia imelengwa, na G7 "imelaani vikali mauzo ya Korea Kaskazini na usambazaji wa makombora ya balestiki ya Korea Kaskazini kwa Urusi" na kutoa wito "kukomeshwa mara moja kwa shughuli hizo"