Coronavirus: Ulaya yachukua hatua kali kujaribu kuzuia kuenea kwa kirusi cha Omicron
Kirusi kipya cha Omicron kinaweza kutawala bara la Ulaya kufikia katikati ya mwezi Januari 2022 kulingana na Rais wa Tume ya Ulaya, Ursula von der Leyen. Katika kujaribu kuzuia kuenea kwake, hatua zinaendelea kuongezeka kote Ulaya.
Imechapishwa:
"Ninapozungumza nanyi, kirusi cha Omicron kinasambaa kwa kasi kubwa kote Ulaya. Kiinaripotiwa hapa, kiko katika nchi yetu, "amesema Michel Martin. Katika hotuba yake siku ya Ijumaa jioni, Waziri Mkuu wa Ireland alitangaza sheria ya kutotoka nje kuanzia saa mbili usiku katika baa, na mikahawa.
Nchini Denmark, kumbi za sinema na kumbi za tamasha zitafungwa Jumapili hii asubuhi. "Katika kipindi cha saa 24 zilizopita, zaidi ya Wadenmark 11,000 wamepima na kupatikana na virusi vya ugonjwa huo. Hiki ndicho kiwango cha juu zaidi tangu kuzuka kwa janga hili. Zaidi ya watu 500 wamelazwa hospitalini. Takwimu za hivi punde zinaonyesha kuwa kirusi kipya cha, Omicron, kinawakilisha kesi moja kati ya tano za maambukizo, "amebaini Waziri Mkuu Mette Frederiksen.
Uingereza pia inakabiliwa na rekodi ya maambukizi ya kirusi hiki kwa siku ya tatu mfululizo na imeamua kuchukua hatua dhidi ya wasafiri kuingia nchini humo. Kwa mfano, haiwezekani kwa Wafaransa, iwe wamechanjwa au la, kuingia nchini Uingereza bila sababu za msingi kuanzia Jumamosi hii usiku wa manane.
Ufaransa inategemea kibali cha chanjo
Huko Ufaransa, serikali inataka kuongeza shinikizo kwa Wafaransa ambao hawajachanjwa dhidi ya Covid-19. Kuingia katika maeneo yaliyo chini ya pasi ya afya, kipimo ambacho kinaonyesha kuwa mtu hajaujaambukizwa hakitatosha tena katika wiki zijazo: itakuwa muhimu kuwa umechanjwa na kupokea kipimo cha nyongeza.
Ujerumani, kwa upande wake, inaandaa orodha ya nchi zilizoko katika "hatari kubwa" ambazo ni pamoja na Ufaransa na Denmark. Wasafiri ambao hawajachanjwa kutoka nchi hizi watalazimika kuheshimu karantini wanapowasili.
Hatua hizi pia huathiri mashindano ya michezo. Hakutakuwa na mechi za raga za Kombe la Ulaya kati ya vilabu vya Ufaransa na Uingereza wikendi hii.