Brexit: Theresa May na Bunge la Uingereza waomba mkataba mpya
Waziri Mkuu wa Uingereza Theresa May anataka kufunguliwa upya mazungumzo na Umoja wa Ulaya. Waziri Mkuu wa Uingereza amewaambia wabunge wa Uingereza kuwa kuna haja ya kuepo kwa mazungumzo mapya na Umoja wa Ulaya.
Imechapishwa:
Hatua hii inakuja wakati Jumanne wiki hii wabunge walipigia kura marekebisho kadhaa ya kuandaa mazungumzo hayo. Licha ya onyo ambalo limekuwa likirejelewa na nchi 27 za Umoja wa Ulaya kuwa makubaliano yaliyokataliwa Januari 15 hayawezi kujadiliwa tena, Bunge la Uingereza bado linaomba mkataba mpya.
Marekebisho hayo yalipigiwa kura na idadi kubwa ya wabunge. Ndio ilipata ushindi wa kura 317 dhidi ya 301 ya Hapana.
Waziri Mkuu Theresa May amekuwa akikabiliwa na shinikizo la kufanyika kwa kura mpya ya maoni kuhusu Uingereza kujitoa katika Umoja wa Ulaya.
Hata hivyo Bi May ameendelea kupinga hoja hiyo akisema kuwa itakuwa ni kweda kinyume na matakwa ya wananchi ambao wengi waliomba nchi yao kujitoa katika Umoja wa Ulaya.