Sudan Kusini yaendelea kukumbwa na mvutano wa uundwaji wa serikali ya umoja
Wananchi wengi nchini Sudan Kusini wameanza kukata tamaa kuhusu kuundwa kwa serikali mpya ya umoja ambayo ingelijumuisha wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na upinzani wenye silaha nchini humo.
Imechapishwa:
Sudani Kusini inakabiliwa na mdororo wa uchumi, na sasa wengi wanaona kwamba mpango wa amani wa nchi hiyo umeanza kufifia.
Baadhi wameendelea kuhoji kama kutakuwa na usalama wa kutosha kwa Riek Machar kurejea nchini humo ifikapo Novemba 12, pale ambapo atahudumu tena kama makamu wa rais wa Salva Kiir.
Moja kati ya masharti ya kiusalama yanayopaswa kufanyika ni kuwepo wanajeshi 3,000 watakaopaswa kumlinda Machar. Upinzani unasema kiongozi huyo hatorudi Sudan Kusini kama jambo hilo halijatekelezwa. Lakini serikali imesema kama upinzani haujarejea nchini humo ni sawa na kuiweka nchi katika usalama mdogo.
Mapema wiki hii SPLM-IO, kundi la waasi linaloongozwa na Riek Machar lilitangaza kwamba “upinzani wenye silaha hautashiriki katika zoezi la kuunda serikali ya umoja wa kitaifa, kama ilivyopangwa mwezi ujao.”
Hivi karibuni Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini, David Shearer alisema mchakato wa amani nchini humo unasalia kuwa, “hatarini, lakini hatua zinapigwa, ” akiongeza kuwa hatua zinategemea u tayari wa pande husika na uungwaji mkono na jamii ya kimataifa katika kuunda serikali ya mpito.