Mchakato wa amani wakumbwa na changamoto mpya Sudani Kusini
Upinzani wenye silaha hautashiriki katika zoezi la kuunda serikali ya umoja wa kitaifa, kama ilivyopangwa mwezi ujao. Kauli hii imetolewa na SPLM-IO, kundi la waasi linaloongozwa na Riek Machar.
Imechapishwa:
Riek Machar na Rais Salva Kiir walitia saini kwenye mkataba wa amani mwaka jana kumaliza miaka 5 ya vita vya wenyewe kwa wenyewe. Watatakiwa kukubaliana kuhusu kugawana madaraka ifikapo Novemba 12.
Tarehe hii iliahirishwa kwa mara ya kwanza. Kwa mujibu wa Puok Both, msemaji wa kundi la waasi la Riek Machar, hawatashiriki katika serikali mpya kama makubaliano yote ya amani hayatatekelezwa.
"Kuna mambo kadhaa muhimu ambayo tunahitaji kushughulikia kwanza, ikiwa tunataka kuleta utulivu nchini na kuwa na serikali ambayo inawatumikia wananchi. Kama kwa mfano maswala ya usalama, idadi ya majimbo, mipaka ya majimbo hayo, na katiba kufanyiwa marekebisho. Tulichelewa sana, na ndio maana tarehe ya mwisho iliahirishwa kwa miezi 6. Kuna sababu kadhaa za kuchelewa kwa mchakato huu, lakini hii ni kwa sababu ya kukosekana kwa utashi wa kisiasa kutoka serikali na ukosefu wa pesa kufadhili mabadiliko haya. Serikali iliahidi kutoa pesa, lakini haijatekeleza ahadi yake. Hii inaonyesha kuwa serikali haina utashi katika mambo hayo. Sote tulisaini makubaliano haya. Na lazima tuweke kando tofauti zetu za kisiasa kwa niaba ya nchi yetu, " amesema Puok Both.
Hivi karibuni Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini, David Shearer alisema mchakato wa amani nchini humo unasalia kuwa, “hatarini, lakini hatua zinapigwa, ” akiongeza kuwa hatua zinategemea u tayari wa pande husika na uungwaji mkono na jamii ya kimataifa katika kuunda serikali ya mpito.