Pata taarifa kuu
UKRAINE

Ukraine yatia saini mkataba wa Kihistoria na Umoja wa Ulaya

Ukraine imetia saini mkataba wa ushirikiano wa kibiashara na kisiasa  na Umoja wa Ulaya jijini Brussels nchini Ubelgiji baada ya mvutano wa muda mrefu kati ya serikali iliyopita na waandamanaji na  kusabibisha machafuko nchini humo.

Jose Manuel Barroso,  rais wa Ukraine  Petro Poroshenko na Herman Van Rompuy
Jose Manuel Barroso, rais wa Ukraine Petro Poroshenko na Herman Van Rompuy REUTERS/Stringer
Matangazo ya kibiashara

Rais wa Ukraine Petro Poroshenko amesema hatua ya nchi yake kutia saini mkataba huo siku ya Ijumaa ni ya Kihistoria na inalenga kuinua uchumi wa nchi hiyo pamoja na kuimarisha uhusiano wake na EU  katika siku zijazo.

“Mkataba huu utaimarisha uhusiano wetu wa kibiashara na kisiasa na Umoja wa Ulaya, na kutoa mtazamo mpya wa nchi yangu,” Poroshenko amesema akiwa Brussels.

“ Ni siku ya Kihistoria, siku muhimu sana tangu Uhuru wetu kutoka kwa Urusi mwaka 1991,” aliongezea.

Petro Poroshenko akitia saini mkataba na Umoja wa Ulaya
Petro Poroshenko akitia saini mkataba na Umoja wa Ulaya REUTERS/Olivier Hoslet

Mbali na Ukraine, Umoja wa Ulaya unatishia mkataba wa ushirikiano na nchi za Georgia na Moldova ambayo ni ishara tosha kuwa mataifa hayo yameamua kushirikiana na mataifa ya Magharibi badala ya Urusi.

Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya Herman Van Rompuy ameyahakikishia mataifa hayo kuwa " Umoja wa Ulaya hautawaacha tutashirikiana nanyi katika maswala mengi na hii ni siku kubwa kwa Umoja wa Ulaya.,"

Mwaka uliopita, hatua ya rais wa zamani wa Ukraine, Viktor Yanukovych kukataa kutia saini mkataba huo na EU ulisababisha maandamano na machafuko nchini humo na kusabisha rais huyo kukimbilia nchini Urusi.

Rais wa Ukraine  Petro Porochenko (katika) akiwa pamoja na Kamishena wa Umoja wa Ulaya  José Manuel Barroso , na rais wa Umoja huo  Herman Van Rompuy, tarehe 27 Juni 2014 wakiwa jijini Brussels
Rais wa Ukraine Petro Porochenko (katika) akiwa pamoja na Kamishena wa Umoja wa Ulaya José Manuel Barroso , na rais wa Umoja huo Herman Van Rompuy, tarehe 27 Juni 2014 wakiwa jijini Brussels REUTERS/Stringer

Kipindi hiki chote Urusi imekuwa ikipinga hatua ya Ukraine kushirikiana na Umoja wa Ulaya badala ya kuegemea upande wao.

Wakati uo huo, viongozi wa Umoja wa Ulaya wameipa Urusi siku tatu kubadilisha sera yake kuhusu Ukraine la sivyo itaiwekea vikwazo zaidi.

Viongozi hao wameitaka Moscow kuja na mbinu kufikia Jumatatu ijayo kumaliza kwa amani la sivyo watachukua hatua zaidi.

Rais wa Urusi Vladimir Putin, amesema hatua ya Ukraine kuingia katika mkataba huo na Umoja wa Ulaya itasababisha nchi hiyo kugawanyika mara mbili.

Umoja wa Mataifa nao unasema watu waliokimbia makwao kutokana na machafuko Mashariki mwa nchi hiyo ni zaidi ya 110,000 wengi wameondoka nchini humo.

 

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.