Michel Kafando: Hali ya kisiasa nchini Burundi bado inalegalega
Mjumbe maalumu wa umoja wa Mataifa kwa nchi ya Burundi Michel Kafando, ambaye ameripotiwa kuachia nafasi yake, amesema hali ya kisiasa nchini Burundi bado si ya kuridhisha kutokana na kile alichosema kukosekana kwa uvumilivu wa kisiasa na kuminywa kwa uhuru wa watu kujieleza.
Imechapishwa:
Kafando, licha ya kupongeza hatua chanya ambazo Serikali ya Gitega imeendelea kuzichukua, ikiwemo kuwa na mazungumzo shirikishi kusaka suluhu ya kudumu, amesema bado mapendekezo mengi hayajatekelezwa.
Kuhusu uchaguzi wa mwakani, Kafando amesema licha ya kuwa suala la uchaguzi ni la nchi na tume ya uchaguzi, ameonya kuwa ikiwa maandalizi yatakuwa ni ya kuzima moto, itakuwa ni chanzo cha vurugu zaidi nchini humo.
Mazungumzo ya amani yaliyodumu kwa karibu miaka minne sasa yameshindwa kutoa suluhu, huku wachambuzi wa masuala ya siasa, wakiionyooshea kidole Jumuiya za Kimataifa kwa kushindwa kumaliza mzozo uliopo Burundi ambao umesababisha mamia ya watu kupoteza maisha na maelfu kuwa wakimbizi.