Nigeria: Karibu wanafunzi 300 watekwa nyara Kaskazini-Magharibi
Nchini Nigeria, mzozo wa kiuchumi unaozidi kuwa mbaya unachangiwa na mzozo wa usalama ambao unaendelea na hata hatari ya kuzorota kutokana na kuzorota kwa hali ya maisha ya watu. Kaskazini-magharibi mwa Nigeria, "majambazi" wameshambulia tena shule ya Kuriga, katika eneo la Kaduna, na kuwateka nyara karibu wanafunzi 300 asubuhi ya Alhamisi Machi 7. Siku hiyo, karibu wanawake 100 waliripotiwa kutoweka.
Imechapishwa:
Na mwanahabari wetu mjini Lagos, Liza Fabbian
Gavana wa Kaduna Uba Sani alitembelea jamii ya Kuriga, ambapo watoto wengi waliotekwa nyara kutoka shule ya eneo hilo siku ya Alhamisi wanatoka. Kulingana na hesabu ya mashahidi, angalau watoto 187 kutoka shule ya sekondari walichukuliwa na watu wenye silaha, pamoja na watoto wengine 125 wa shule ya msingi - 25 kati yao walifaulu kutoroka. Walimu pia hawajulikani waliko.
Katika miaka ya hivi majuzi, utekaji nyara mkubwa unaolenga shule umekuwa ukitokea mara kwa mara katika jimbo la Kaduna. Makundi ya wenyeji wenye silaha pia huwashambulia mara kwa mara wakulima au wasafiri wanaotoka nje ya miji. Na mara nyingi familia huachiwa wenyewe kufanya mazungumzo na majambazi hawa, kisha kulipa fidia wanazodai.
Mashariki mwa Nigeria, katika jimbo la Borno, lililosambaratishwa kwa zaidi ya muongo mmoja na ghasia za wanajihadi, hali ya usalama pia inatia wasiwasi. Siku ya Alhamisi, Machi 7, mamlaka ilithibitisha utekaji nyara wa makumi ya wanawake katika eneo la Ngala, eneo lililo karibu na mpaka wa Cameroon: angalau wanawake 100 ambao walikuwa wameenda kutafuta kuni hawakurudi kwenye kambi ya watu waliokimbia makazi wanakoishi.
Licha ya kuendelea kuwepo kwa wanajihadi kutoka Boko Haram na ISWAP (kundi la Islamic State Afrika Magharibi) katika eneo hilo, mamlaka ya eneo hilo ilianza mwaka 2021 kuwarejesha watu waliokimbia makazi yao katika vijiji vyao wanakotoka.