Mkutano wa kimataifa kuhusu Libya kufanyika Januari 19 Berlin
Mkutano wa kimataifa kuhusu hali inayoendelea nchini Libya utafanyika Januari 19 mwaka huu jijini Berlin, serikali ya Ujerumani imebainisha Jumanne wiki hii.
Imechapishwa:
Mkutano huo utawaleta pamoja wawakilishi kutoka Marekani, Urusi, China, Ufaransa, Uturuki, Uingereza na Italia, serikali ya Ujerumani imesema, na kuongeza kuwa Waziri Mkuu wa Libya Fayez al Sarraj na mbabe wa kivita Mashariki mwa Libya Marshal Khalifa Haftar pia wamealikwa katika mkutano huo.
Hayo yanajiri wakati mazungumzo yaliyofanyika tangu Jumatatu katika mji mkuu wa urusi, Moscow kwa jitihada za Urusi na Uturuki yamekwenda kombo. Hayo ni baada ya mbabe wa kivita Mashariki mwa nchi hiyo, Marshal Haftar kuondoka Urusi bila kusaini makubaliano ya kusitisha mapigano.
Jumatatu jioni wiki hii kiongozi wa serikali inayotambuliwa na Umoja wa Mataifa Fayez al-Sarraj, alitia saini mkataba wa makubaliano ya kusitisha vita, lakini mpizani wake, Khalifa Haftar aliomba muda zaidi kupitia makubaliano hayo.
Haijajulikana ni kwa nini alifutilia mbali ya kusitisha mapigano. Lakini kwa mujibu wa vyanzo kadhaa kutoka kambi ya Khalifa Haftar, hatua ya mbabe huyo wa kivita ilisababishwa na jukumu la Uturuki kutamka wazi kwamba yuko tayari kutuma askari nchini Libya kusaidia serikali ya Tripoli inayoongozwa na Fayez el-Sarraj.