Nhlanhla Nene: Nilifutwa kazi na Zuma kwa kukataa rushwa
Waziri wa Fedha wa Afrika Kusini ametoa ushuhuda wake Jumatano wiki hii kuwa alifutwa kazi miaka mitatu iliyopita na rais wa zamani Jacob Zuma kwa kukataa kutekeleza maamuzi kwa faida ya familia ya Gupta, baada ya familia hiyo kuhusishwa na kashfa za rushwa nchini.
Imechapishwa:
"Nadhani niliachishwa kazi kwa sababu ya kukataa kwangu kuweka katika vitendo baadhi ya maamuzi," Nhlanhla Nene ameiambia tume inayohusika na kuchunguza mambo ya kisiasa na kifedha yaliyosababisha Zuma. kushinikizwa ajiuzulu mnamo mwezi Februari.
"Nikikumbuka vizuri maamuzi hayo yaliinufaisha familia ya Gupta na watu wengine ambao ni washirika wa karibu sana na rais Zuma," ameongeza.
Bw Nene alitimuliwa kwenye wadhifa wake na Jacob Zuma mwezi Desemba 2015, uamuzi ambao wakati huo ulisababisha mdororo wa masoko ya kifedha.
Mrithi wa Bw Zuma, Cyril Ramaphosa, alimrejesha kwenye nafasi yake baada ya kuchukua hatamu ya uongozi wa nchi.
Jacob Zuma anashtumiwa kuwa katika muhula wake wa pili (2009-2018) aliipa mikataba mikubwa ya fedha nyingi familia ya Gupta. Hata hivyo Jacob Zuma amekuwa akikanusha madai hayo, lakini akikiri kuwa alikuwa karibu na wafanyabiashara watatu kutoka familia hiyo.