Kanisa katoliki latoa wito kwa mazungumzo nchini Burundi
Kanisa Katoliki nchini Burundi limetoa wito kwa serikali ya nchi hiyo kuanzisha mazungumzo na upinzani ili kuwezesha kurudi kwa maelfu ya wakimbizi wa Burundi waishio uhamishoni.
Imechapishwa:
Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki nchini Burundi, Gervais Banshimiyubusa amesema kuwa mazungumzo yanaihitajika ili kumaliza mgogoro huo.
"Wakati wanasiasa wataendelea kuwachukulia wale ambao si kutoka kambi yao kama maadui, mazungumzo hayatawezekana," Askofu Banshimiyubusa amesema.
"Watu hawakai na maadui zao, badala yake wanawakimbia," ameongeza.
Spika wa Bunge ajitetea
Hali ya kisiasa imeimarika na inatosha tu kuwajulisha wakimbizi ili waweze kurudi nyumbani, Spika wa Bunge la Burundi Pascal Nyabenda aliwaambia Maaskofu Jumapili Novemva 20 wakati wa sherehe za kidini.
Visa vya ukandamizaji vinavyoendeshwa na utawala tangu Rais Pierre Nkurunziza kuchukua uamuzi, mwezi Aprili mwaka 2015, wa kuwania muhula mwingine, vimeendelea kushuhudiwa nchini humo.
Baadhi ya wafuasi wa chama tawala walishambuliwa na kunyanyaswa na watu ambao hawakuweza kujulikana.
Kwa hofu ya kuuawa, maelfu ya wananchi wa Burundi, ikiwa ni pamoja wanaharakati wa haki za binadamu na wanasiasa wa upinzani, walikimbilia katika nchi jirani, hasa nchini Rwanda na Tanzania.
Kwa mujibu wa shirika la kuhudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa, zaidi ya Warundi 200,000 wameitoroka nchi yao katika kipindi cha miezi 19 iliyopita.