Mashambulizi ya Marekani Iraq: Waandamanaji wavamia ubalozi wa Marekani
Vifo vya wapiganaji 25 wanaounga mkono serikali ya Iran katika shambulio la kulipiza kisasi la Marekani siku ya Jumapili vimesababisha hasira nchini Iraq.
Imechapishwa:
Kutokana na hali hiyo waombolezaji wamekusanyika nje ya ubalozi wa Marekani mjini Baghdad kulaani mashambulio ya ndege za Marekani yaliyolenga vituo vya wanamgambo wa Kishia.
Waombolezaji hao walizingira ubalozi huo uliopo kwenye eneo lenye ulinzi mkali wakiwa wamebeba bendera za kundi la wanamgambo lenye ushawishi mkubwa.
Wadadisi wanabaini kwamba makabiliano hayo kati ya Marekani na wanamgambo wanaoungwa mkono na Tehran inaonyesha jinsi gani serikali haina nguvu ya kuhakikisha uhuru wa Iraq, wakati nchi hiyo inakabiliwa na maandamano ya kiraia ambao wanaomba wanasiasa wote kwa jumla wajiuzulu kwenye nafasi zao.
Kwa upande mwengine Saudi Arabia imewalaani wanamgambo wanaoungwa mkono na Iran kwa kuyashambulia majeshi ya Marekani yaliyoko nchini Iraq ambapo mkandarasi mmoja wa Marekani aliuliwa.
Wanamgambo hao walifanya mashambulio hayo wiki iliyopita. Marekani ilijibu kwa kuwashambulia kwa ndege wanamgambo hao wa Kataib Hezbollah Jumapili iliyopita. Wanamgambo hao wa Hezbollah walikishambulia kituo cha kijeshi cha Marekani nchini Irak Ijumaa iliyopita.