Mvutano waendelea Lebanon, utawala washindwa kudhibiti hali ya mambo
Maandamano makubwa ya kiraia yanaendelea kwa siku ya 15 mfululizo nchini Lebanon, licha ya Waziri Mkuu Saad Hariri kujiuzulu Jumanne wiki hii. Waandamanaji wanalalamikia hali ya uchumi na maisha kuendelea kuwa mbaya zaidi katika taifa hilo la Kiarabu.
Imechapishwa:
Miji mbali mbali ya Lebanon na hasa mji mkuu Beirut imekuwa ikishuhudia maandamano ya kupinga serikali wanaolalamikia utendaji dhaifu wa serikali kuhusiana na hali ya maisha na uchumi pamoja na kodi mpya zilizotangazwa na serikali hiyo iliyojiuzulu.
Hayo yakijiri Rais wa Lebanon Michel Aoun ameliomba baraza lake la mawaziri kuendelea kuiongoza serikali ya mpito hadi pale serikali mpya itakapoundwa kufuatia kujiuzulu Waziri Mkuu Saad al Hariri pamoja na serikali yake siku ya Jumanne.
Hata hivyo afisa mmoja mwandamizi aliye karibu na Hariri amesema waziri mkuu huyo yupo tayari kurejea tena kwenye wadhifa wake lakini kwa masharti ya kujumuishwa wasomi watakaoweza kutekeleza mabadiliko yanayohitajika ya kuuokoa uchumi wa nchi hiyo unaoyumba.
Afisa huyo ambaye hakutaka kutambulishwa amesema baraza la mawaziri litatakiwa kutowajumuisha wanasiasa waliokuwa katika serikali inayoondoka.
Hariri amejiuzulu baada ya kushindwa majaribio yake ya kuutatua mgogoro wa kiuchumi hali iliyochochea maandamano makubwa ya siku 13 dhidi ya serikali yake.