Urusi kuimarisha mfumo wake wa ulinzi Syria
Urusi imetangaza mikakati mipya ya usalama kuwalinda wanajeshi wake nchini Syria. Hayo yanajiri wakati ambapo kulikuwa na hali ya sintofahamu baada ya ndege ya Urusi kuangushwa na majeshi ya Syria wiki iliyopita.
Imechapishwa:
Waziri wa Usalama Sergei Shoigu amesema rais Vladimir Putin amemwagiza kuwa na ndege maalum ya kuchunguza operesehni za kijeshi zinazoendelea.
Hatua hii imekuja baada ya jeshi la Syria wiki iliyopita kuiangusha ndege ya Urusi na kusababisha vifo vya watu 15.
Mapema wiki iliyopita Rais wa Urusi Vladimir Putin alisema kuangushwa kwa ndege ya kijeshi ya nchi yake na wanajeshi wa Syria, lilikuwa ni tukio lililotokea kwa bahati mbaya.
Kauli hii imekuja, baada ya wizara yake ya ulinzi kuishtumu Israel kwa kuiangusha ndege hiyo na kusababisha wanajeshi wote 15 wa Urusi kuangamia.
Matamshi ya rais Putin yalilenga kutoharibu uhusiano kati ya nchi yake na Syria.
Israel imekuwa ikitishia kuwa itaangusha ndege yoyote ya kivita, itakayoonekana katika anga lake kwa sababu za kiusalama.
Syria imekuwa ikisema Israel ni adui wake na ndio sababu ililenga ndege hiyo, ikifikiria ni ya Israel.
Urusi ilituma wanajeshi wake nchini Syria mwaka 2015, kusaidia serikali ya rais Bashar Al Assad kupambana na makundi ya kigaidi.