Putin: Jeshi la Urusi halijandoka Syria kwa sasa
Rais wa Urusi Vladimir Putin amesema, hakuna wa kuliagiza jeshi la nchi yake kuondoka nchini Syria kwa sasa. Hata hivyo, amesema Urusi haina mpango wa kujenga kituo cha kudumu cha kijeshi nchini Syria.
Imechapishwa:
Putin ameongeza kuwa jeshi lake limepata uzoefu wa kipekee nchini Syria na kusisitiza kuwa kuwepo kwao katika nchi hiyo ni kutekeleza majukumu yao ya Kimataifa.
Hayo yanajiri wakati ambapo mapigano yanaendelea kurindima nchini Syria. Kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka miwili, wapiganaji wa kundi la Islamic State (IS) wameonekana katika jimbo la kusini la Soueida, nchini Syria. Wapiganaji wasiopungua 17 kutoka kundi linalounga mkono serikali waliuawa siku ya Alhamisi, Juni 7 katika mashambulizi yaliyoendeshwa na wanamgambo wa kiislamu, kwa mujibu wa shirka la Haki za Binadamu nchini Syria (OSDH). Jeshi la Syria limeanzisha operesheni kabambe katika eneo hilo.
Baada ya kupoteza ngome yake ya mwisho ya Hajar al-Aswad na kambi yake ya Yarmouk katika mji wa Damascus Mei 22,IS imeongeza mashambulizi yake dhidi ya jeshi la Syria na washirika wake. Wapiganaji wa kundi hili waliendesha mashambulizi makubwa matatu karibu na mji wa kale wa Palmyra na katika jimbo la mashariki la Deir Ezzor.
OSDH inasema kuwa wapiganaji 180 wa makundi yanayounga mkono serikali waliuawa katika mashambulizi hayo. Askari wanne kutoka Urusi pia ni miongoni mwa waliouawa.
Kundi la Islamic State bado lina nguvu kubwa katika jangwa la Badia, ambalo linaendelea hadi kwenye mpaka wa Iraq.