Kanisa Katoliki latilia shaka ushindi wa Jenerali Ndayishimiye katika uchaguzi wa rais Burundi
Maaskofu wa Kanisa Katoliki nchini Burundi wanasema, Uchaguzi Mkuu uliofanyika wiki iliyopita, uligubikwa na udanganyiku mkubwa na hivyo wanatilia shaka ushindi wa mgombea wa chama tawala, Evariste Ndayishimiye aliyetangazwa mshindi na Tume ya Uchaguzi wiki hii.
Imechapishwa:
Baraza la maaskofu hao, limeongeza kuwa waangalizi wake waliokuwa katika vituo mbalimbali vya kupigia kura kote nchini, walishuhudia kuhitilafiwa kwa masanduku ya kupigia kura na kutishwa kwa wapiga kura.
Ripoti hii ya maaskofu inakuja siku chache baada ya Tume Huru ya Uchaguzi nchini Burundi, CENI, kumtangaza Jenerali Evariste Ndayishimiye mshindi katika uchaguzi wa urais uliofanyika Jumatano Mei 20, 2020 kwa kupata 68.72% ya kura dhidi ya mshindani wake mkuu Agathon Rwasa aliyepata 24.19% ya kura.
Mapema wiki hii Chama cha CNL cha Agathon Rwasa kilitangaza kwamba kitawasilisha malalamiko yake katika Mahakama ya Katiba kupinga matokeo ya uchaguzi huo, kikisema kuwa ni uchaguzi ambao uligubikwa na udangayifu mkubwa.
Iwapo Mahakama ya Katiba itahibitisha matokeo ya uchaguzi Jenerali Evariste Ndayishimiye atakuwa rais wa tatu aliyechaguliwa chini ya misingi ya kidemokrasia tangu nchi hiyo kupata uhuru wake Julai 1, 1962, na hivyo kuchukuwa mikoba ya mtangulizi wake Pierre Nkurunziza kutoka chama cha CNDD-FDD.
Hayo yanajiri wakati wanadilpomasia wa nchi za kigeni nchini Burundi wanasema wamepokea taarifa ya ushindi wa Jenerali Evariste Ndayishimiye bila hata hivyo kuzungumza lolote kuhusu madai ya wizi wa kura yaliyotolewa na Agahton Rwasa.
Tayari rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Felix Tshisekedi ametoa salamu za pongezi kwa rais mteule wa Burundi Jenerali Evariste Ndayishimiye akimuomba kutoa ushirikiano wake kwa usalama wa kanda nzima ya maziwa makuu.
#RDC 26.05.20|Le Chef de l’État S.E.M Félix-Antoine Tshisekedi a félicité le nouveau Président du #Burundi,#EvaristeNdayishimiye. Le Président congolais a assuré son homologue de sa disponibilité «à œuvrer ensemble pour la paix et le développement dans la région des Grands Lacs».
Présidence RDC 🇨🇩 (@Presidence_RDC) May 26, 2020