Pata taarifa kuu
BURUNDI-USALAMA-SIASA

Warundi waadhimisha miaka 29 ya umoja wao

Huu ni mwaka wa 29 toka makabila tofauti ya Warundi kukubaliana kwa pamoja kudumisha umoja wao baada ya makabila mawili makubwa (Wahutu na Watutsi) kuendelea kutengana kwa miaka mingi, kila upande ukishtumu upande mwengine kuwa ni adaui yake.

Mnara wa umoja wa Warundi, Bujumbura.
Mnara wa umoja wa Warundi, Bujumbura. Tourisme.gov.bi
Matangazo ya kibiashara

Kila tarehe 5 Februari Warundi wanasherehekea umoja wao. Tarehe hii inafika wakati Uchaguzi Mkuu unatarajiwa kufanyika mwezi Mei na mrithi wa rais Pierre Nkurunziza atapatikana.

Licha ya tofauti za kikabila ambazo zipo Warundi kwa sasa wameshikamana, ukilinganisha na miaka ya 1990, ambapo watu kutoka jamii ya walio wachache (Watutsi) walitawala Burundi kwa miaka mingi kabla na baada ya uhuru hadi miaka ya 1993.

Katika miaka 1988 na 1990 kulikuwa na machafuko mbalimbali na watu kadhaa waliuawa katika machafuko hayo, wengi wao kutoka kabila la walio wengi (Wahutu).

Kutokana na hali hiyo rais wa zama hizo Pierre Buyoya, kutoka kabila la walio wachache (Watutsi) na waziri wake mkuu Adrien Sibomana kutoka kabila la walio wengi (Wahutu) waliafikiana kuwaleta pamoja Warundi kutoka makabila mbalimbali licha ya tofauti zao.

Wawili hao walianza mchakato wa kutafuta maridhiano kati ya makabila hayo mawili hasimu (Wahutu na Watutsi).

Baada ya mchakato huo pande zote mbili zilifikia makubaliano na kile kilichosainiwa kiliitwa Makubaliano ya Umoja wa Warundi “Amasezerano y'Ubumwe bwa Barundi”.

Kwa sasa hali ya Bujumbura na maeneo mengine nchini ni shwari.

Pamoja na kwamba kulikuepo na makubaliano ya umoja, baadhi ya wadadisi wanabaini kwamba makubaliano hayo hayakukamilika au hayakufikia malengo yake kama ilivyotarajiwa na wengi, kwa sababu miaka miwili baadae kulitokea machafuko mengine, ambapo Melchior Ndadaye, rais wa kwanza kutoka kabila la Wahutu aliyechaguliwa kupitia mfumo wa vyama vingi, aliuawa.

Tanzania na jumuiya ya kimataifa walisimama na kuwashinikiza Warundi kuboresha maridhiano na kushikamana. Hatimaye Warundi walifikia makubaliano na kutia saini kwenye mkataba uliitwa Mkataba wa Amani wa Arusha.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.