Kenya: Shule ya msingi ya Precious Talents yafungwa baada ya vifo vya wanafunzi saba
Serikali ya Kenya imefunga shule ya msingi ya kibinafsi ya Precious Talents iliyopo jijini Nairobi baada ya darasa kuporomoka na kusababisha vifo vya wanafunzi saba jana asubuhi.
Imechapishwa:
Wakati huo watato zaidi ya 60 waliokuwa wamekimbizwa hospitalini baada ya mkasa huo wameruhusiwa kwenda nyumbani, baada ya kupata nafuu.
Mkasa huo ulitokea wakati wanafunzi hao walipokuwa wameingia darasani wakisubiri kuanza masomo yao katika shule hiyo binafsi inayoitwa Precious Talent.
Awali msemaji wa serikali Cyrus Oguna alisema wanafunzi 57 wamelazwa katika Hospitali Kuu ya Kenyatta wanakoendelea kupata matibabu.
Mamia ya wakaazi wa mtaa huo na wazazi waliokuwa wa kwanza kufika katika eneo hilo la mkasa walionekana wenye hasira kwa kile walichokisema, maafisa wa serikali ya Kaunti ya Nairobi walichukua muda mrefu kufika katika shule hiyo kuwaokoa wanafunzi hao.
Imebainika kuwa, ujenzi wa Shule hiyo haukuwa imara kwa sababu ilijengwa kwa vifaa duni vya ujenzi, yakiwemo mabati na mbao.
Shule hiyo ina wanafunzi zaidi ya 800, kutoka mtaa huo wenye watu wanaoishi katika maisha magumu.