Mahakama ya Juu nchini Uganda yafanya uamuzi wa kumwezesha rais Museveni kuwania tena
Mahakama ya Juu nchini Uganda imeamua kuwa bunge lilifuata sheria wakati wa kuondoa kipengelee tata cha ukomo wa mtu anayetaka kuwania urais nchini humo, uamuzi ambao unampa nafasi rais Yoweri Museveni mwenye umri wa miaka 74, kuendelea kutafuta urais mwaka 2021.
Imechapishwa:
Wakiongozwa na Jaji Mkuu Bart Katureebe, Majaji wanne walitupilia mbali kesi hiyo ya upinzani huku Majaji watatu wakisema bunge halikufuata sheria wakati wa mabadiliko hayo.
“Kesi hii, haijakubaliwa,”amesema Jaji Mkuu Katureebe katika Mahakama ya Juu jijini Kampala.
Uamuzi huu unampa nafasi kwa rais Museveni ambaye amekuwa akiongoza nchini hiyo tangu mwaka 1986, na ana nafasi ya kuwania tena mwaka 2021 na kuendelea hadi mwaka 2026.
Mwanasheria Mkuu wa serikali Mwesigwa Rukutana amesema uamuzi huo wa Mahakama ni ushindi kwa wananchi wa Uganda.
Haya hivyo, wakili wa upinzani Erias Lukwago, amesema demokrasia ipo katika hali ngumu.
“Ni masikitiko makubwa lakini barani Afrika, ni miujiza kushinda dhidi ya serikali iliyo madarakani, aliongeza Lukwago.