Mfalme wa Jordan Abdullah wa pili azuru Kenya
Mfalme wa Jordan Abdullah wa pili anazuru Kenya.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Abdullah aliwasili jijini Nairobi Jumatatu mchana na kukaribishwa na mwenyeji rais Uhuru Kenyatta, aliyekuwa amevalia sare ya kijeshi sawa na mgeni wake.
Viongozi hao wa wawili wameshuhudia mazoezi ya pamoja ya kijeshi kati ya wanajeshi wa nchi hizo mbili katika kambi ya kijeshi ya Embakasi jijini Nairobi, mazoezi ambayo yamekuwa yakiendelea kwa siku kadhaa.
Mbali na kushuhudia mazoezi hayo ya kijeshi, viongozi hao wanatarajiwa kujadili maswala ya kiusalama hasa kuhusu namna ya kushinda ugaidi lakini pia ushirikiano wa kibiashara .
Kenya imeendelea kukabiliana na tishio la ugaidi kutoka kundi la Al Shabab kutoka nchini Somali baada ya kutuma jeshi lake nchini humo mwka 2011.
Jordan imeendelea kuisaidia Kenya kupambana na ugaidi hasa kuhusu maswala ya kiiteljensia na mbinu za kisasa za kukabiliana na ugaidi.
Mbali na ziara ya Mfalme Abdullah wa pili, Ikulu ya Nairobi imetangaza kuwa rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma anatarajiwa kuzuru nchi hiyo mwezi ujao kujadili maswala mbalimbali.