Wakuu wa EAC kukutana Dar es Salaam, Burundi, Sudan Kusini kuwa ajenda
Wakuu wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki, EAC, wanatarajiwa kukutana mwishoni mwa juma hili jijini Dar es Salaam, nchini Tanzania, kuanzia September 8 hadi 9, ambapo masuala kadhaa yanatarajiwa kujadilia.
Imechapishwa:
Mkutano huu wa dharura wa 17 wa wakuu wa nchi za Afrika Mashariki, utafanyika wakati huu nchi ya Sudan Kusini ikiwasilisha rasmi barua ya utambulisho wa kuwa kwenye kamati ya utendaji na maamuzi ya jumuiya hiyo, baada ya kutia saini itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Kwenye mkutano huu, wakuu wa nchi za Afrika Mashariki watapokea na kujadili ripoti ya baraza la mawaziri wa nchi wanachama kuhusu makubaliani ya ushirikiano wa kiuchumi baina ya nchi hizo na Jumuiya ya umoja wa Ulaya.
Mbali na ajenda kuhusu ushirikiano wa kiuchumi na nchi za Ulaya, wakuu hao pia watapokea ripoti ya Rais wa zamani wa Tanzania, Benjamini Mkapa kuhusu maendeleo ya mazungumzo ya amani ya kitaifa kwa nchi ya Burundi, mazungumzo ambayo mpaka sasa hayajoa muelekeo wa kupatikana kwa suluhu.
Ajenda nyingine ambayo itajadiliwa na wakuu hao wa nchi ni pamoja na kupokea ripoti ya tathmini ya mambo yanayojiri kwenye taifa la Sudan Kusini, ambapo pia watapokea rasmi barua ya taifa hilo kutaka kushirikishwa kwenye kamati ya maamuzi ya juu ya jumuiya hiyo baada ya kuwa mwanachama.
Kuapishwa kwa naibu katibu mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, ni tukio jingine ambalo litatekelezwa na viongozi hao.
Mkutano huu unafanyika wakati ambapo hali ya mambo nchini Sudan Kusini, mwanachama mpya kabisa wa Jumuiya ikiwa bado ni tete, huku utekelezaji wa mkataba uliotiwa saini mwaka jana kati ya Rais Salva Kiir na hasimu wake Riek Machar ukiwa bado unasuasua.