Kenya: Zaidi ya raia milioni nne bado wanakabiliwa na baa la njaa: WFP
NAIROBI – Licha ya kuwa mvua imeanza kushuhudiwa katika baadhi ya maeneo nchini Kenya, zaidi ya raia milioni nne katika taifa hilo la Afrika Mashariki bado wanakabiliwa na athari za baa la njaa kwa mujibu wa takwimu za shirika la mpango wa chakula duniani WFP.
Imechapishwa:
Shirika la WFP linaongeza hatua zake za dharura kusaidia mamia kwa maelfu ya Wakenya walioathiriwa na athari za takriban miaka mitatu ya ukame.
Shirika hilo linalenga kusaidia zaidi ya watu 940,000 walioathiriwa na ukame - ongezeko kutoka karibu watu 600,000 katika mwaka wa 2022.
Ukame wa muda mrefu zaidi katika historia ya Pembe ya Afrika, umewaacha watu milioni 4.4 nchini Kenya wakikabiliwa na njaa. Takriban watoto na wanawake milioni 1.5 wana utapiamlo na karibu mifugo milioni 3 wamekufa.
Kupitia kwa mpango wake wa lisha jamii, WFP inalenga kuwafikia raia hao wanaokabiliwa na baa la njaa hadi pale wakulima wataanza kuvuna mimea yao. Walionufaika na mpango huo ni raia wa Trukana, kaskazini mashariki mwa taifa hilo.
Shirika hilo la umoja wa mataifa kwa ushirikiano na USAID linalenga kuzisaidia familia zilizoathirika kwa kuwapa fedha, vyakula kama vile mtama, mafuta ya kupika, mchele na mawele kwa kipindi cha miezi sita.
Serikali ya Kenya kwa ushirikiano na mashirika mengine ya misaada, nayo pia imeanzisha mchakato wa kuwasaidia raia wake wanaokabiliwa na njaa.