Nchi za G7 zakutana kujadili masuala mbalimbali yanaoikumba dunia
Mawaziri wa Mambo ya Nje kutoka mataifa tajiri duniani ya G7, wanakutana jijini London nchini Uingereza, kikao cha kwanza cha ana kwa ana kinachofanyika kwa mara ya kwanza baada ya dunia kukabiliwa na janga la COVID-19.
Imechapishwa:
Kikao hicho kimewakutanisha Mawaziri wa Mambo ya nje kutoka Ufaransa, Canada, Ujerumani, Italia, Japan, Uingereza na Marekani.
Miongoni mwa ajenda kubwa za kikao hicho ni jitihada za dunia katika kupambana na janga la COVID-19 wakati huu nchi ya India ikielemewaΒ na maambukizi ya Corona.
Mkutano huu unakuja wakati huu mataifa tajiri yakiongozwa na Marekani yakiendelea kuwa na uhusiano baridi na nchi ya Urusi pamoja na China.
Mambo mengine yanayojadiliwa na Mawaziri hao wa Mambo ya nje ni mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabia nchi lakini pia utekelezwaji wa mkataba wa Nyuklia kuhusu Iran ambao Marekani ilijiondoa wakati wa uongozi wa rais Donald Trump.
Mkutano huu ni maandalizi ya mkutano wa wakuu wa nchi hizo, utakaofanyika mwezi Aprili, nchini Uingereza na itakuwa ziara ya kwanza nje ya nchi kwa rais wa Marekani Joe Biden.