Donald Trump: Muda umewadia wa kutumia nguvu dhidi ya Korea Kaskazini
Wakati akikamilisha ziara yake nchini Koarea Kusini, Rais wa Marekani Donald Trump ameitahadharisha Korea Kaskazini kutoendelea kudharau jamii ya kimataifa.
Imechapishwa:
Rais Trump ametoa onyo kali kwa kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong-un kuwa muda umewadia wa kukabiliana naye.
“Silaha unazojilimbikia hazikufanyi wewe kuwa salama lakini zinakuweka katika hali hatari”, amesema Rais Donald Trump katika hotuba yake.
Bw. Trump amesema “dunia haiwezi kuvumilia hatari inayosababishwa na taifa linaloongozwa na utawala usioaminika ambao unaitishia na silaha za kinyuklia”.
“Mataifa yote yaliowajibika yanafaa kuungana kuangamiza utawala wa kikatili wa Korea Kaskazini kuhakikisha kuwa hakuna mtu anayeuunga mkono, kupata usaidizi wowote ama hata kukubalika, “ rais Donald trump ameongeza.
Awali Rais wa Marekani Donald Trump aliitaka Korea Kaskazini kuja kwenye mazungumzo kujadili suala la kuondoa silaha za nyuklia.
Donald Trump ameutaka ulimwengu hususan China na Urusi kuiwekea shinikizo kali Pyongyang kusitisha utengenezaji wake wa silaha za kinyuklia.
Rais Donald Trump amehitimisha ziara ya siku mbili nchini Korea Kusini katika ziara ya bara Asia na anaelekea China.