Washington na Moscow watia mbele ushirikiano licha ya "tofauti kubwa" kati yao
Waziri wa Mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken na Waziri wa Mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov wote wawili wamebaini kwamba tofauti zipo kati ya Marekani na Urusi lakini kwamba nchi hizo zinapaswa kushirikiana katika maswala kadhaa.
Imechapishwa:
Antony Blinken amesema Joe Biden anataka "uhusiano wa kweli na thabiti na Urusi" na kwamba nchi hizo mbili zinaweza kufanya kazi pamoja kupambana na janga la COVID-19, kupambana na Tabia nchi, kukabiliana na mipango ya nyuklia ya Iran na Korea Kaskazini, na vita vya Afghanistan.
"Tunaamini ni vizuri kwa raia wetu, ni vizuri kwa raia wa Urusi na ni vizuri hata kwa ulimwengu," amesema waziri wa mambo ya nje wa Marekani.
Sergei Lavrov amesema mazungumzo hayo yalikuwa "mazuri" na kwamba wanadiplomasia hao wawili wataandaa mapendekezo ya mkutano unaowezekana kati ya Rais wa Marekani Joe Biden na Rais wa Urusi Vladimir Putin, kulingana na vyombo vya habari vya serikali ya Urusi.
Nusu saa baada ya mkutano wa Jumatano kuanza, Marekani iliweka vikwazo kwa meli na makampuni yanayohusika katika ujenzi wa bomba la mafuta, mradi utakaogharimu dola bilioni 11 la Nord Stream 2 ambalo lingebeba gesi Urusi kutoka Arctic kwenda Ujerumani, mpango ambao Joe Biden alipinga. Walakini, utawala umeamua kuondoa vikwazo dhidi ya kampuni inayosimamia mradi huo na mkurugenzi wake mkuu.
Sergei Lavrov hakujibu maswali juu ya vikwazo hivyo. Kabla ya tangazo hilo, Naibu Waziri wa Mambo ya nje wa Urusi Sergei Ryabkov amesema kuondoa vikwazo hivi kutasaidia kurekebisha uhusiano kati ya Moscow na Washington.