Upinzani nchini Ecuador wasema mgombea wake ameibiwa kura za urais
Mgombea wa upinzani nchini Ecuador, Guillermo Lasso amedai kuibiwa kura katika Uchaguzi wa duru ya pili uliofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita dhidi ya mpinzani wake Lenin Moreno.
Imechapishwa:
Moreno alitangazwa mshindi baada ya kupata asilimia 51.12 ya kura zote dhidi ya Lasso aliyepata asilimia 48.88.
Mgombea huyo wa upinzani anasema ana ushahidi kuwa kura zake ziliibiwa ili kumpa ushindi Moreno ambaye alikuwa Makamu wa rais wa Rafael Correa anayeondoka madarakani tangu mwaka 2007.
Uchaguzi nchini Ecuador umekuwa kama kipimo cha demokrasia katika eneo la Latin America, wakati huu mgombea wa upinzani akitaka kura kuhesabiwa upya.
Licha ya Tume ya Uchaguzi kutangaza matokeo hayo, Lasso na Moreno wamesema wote ni washindi hali ambayo inatarajiwa kuzua mvutano mkali wa kisiasa nchini humo katika siku zijazo.
Hata hivyo, ushindi wa Moreno ni faraja kubwa sana kwa Julian Assange mmiliki na mwanzilishi wa tovuti ya Wikileaks aliyepewa hifadhi katika Ubalozi wa Ecuador nchini Uingereza.
Wakati wa kampeni, Moreno aliahidi kuendelea kumpa hifadhi Assange anayetafutwa kwa madai ya ubakaji, huku Lasso akiapa kumwondoa katika Ubalozi huo.