Gavana wa jimbo la North Carolina atangaza hali ya hatari
Gavana wa jimbo la North Carolina ametangaza hali ya hatari Jumatano wiki hii kwa sababu ya vurugu ambazo zinaendelea kuukumba mji wa Charlotte unaokabiliwa na maandamano, yaliyosababishwa na kifo cha mtu mweusi aliuawa na polisi.
Imechapishwa:
Mji wa Charlotte umeendelea kukumbwa Jumatano na machafuko katika usiku wa pili mfululizo. Mtu mmoja alijeruhiwa na yuko katika hali mbaya, baada ya vurugu "kati ya raia," kwa mujibu wa manispaa ya jiji. Polisi ilitumia risasi za mpira na mabomu ya kutoa machozi kwa kuwatawanya waandamanaji.
Maandamano makubwa yalizuka katika mji Jumanne wiki hii baada ya askari polisi kumuua kwa kumpiga risasi mtu huyo mweusi. Kwa mujibu wa askari aliyeendesha kitendo hicho, mtu huyo aliyeuawa alikuwa na silaha aina ya bastola katika kituo cha magari ambapo polisi ilikua ikimtafuta mtuhumiwa.
Waandamanaji wameendelea kukusanyika jirani na maduka makubwa mjini Charlotte ambako tukio hili lilitokea, wakiwa wamebeba mabango yanayosomeka “Black Lives Matter” wakiimba “hakuna haki! Hakuna amani!”.
Taarifa kutoka kwenye mji huo zinasema kuwa mtu aliyepigwa risasi na Polisi wa kituo cha Charlotte-Mecklenburg, ametambuliwa kwa jina la Keith Lamont Scott.
Mkuu wa kitengo cha Polisi cha Charlotte-Mecklenberg, amethibitisha kifo cha kijana huyo na kuongeza kuwa Polisi wake wanne walijeruhiwa wakati wa makabiliano na waandamanaji.
Taarifa zaidi kutoka kwenye mji huo zinasema kuwa Polisi, Brentleu Vinson aliyehusika kwenye tukio hilo, tayari amepewa likizo yenye malipo wakati huu uchunguzi ukiendelea.
Tukio hili linajiri ikiwa imepita miezi kadhaa toka kushuhudiwa kwa maandamano kama haya nchini Marekani, kupinga vitendo vya ubaguzi vinavyodaiwa kutekelezwa na Polisi weupe dhidi ya vijana weusi.