Kenya: Odinga atilia shaka uamuzi wa kutumwa kwa polisi nchini Haiti
Nairobi – Kiongozi wa upinzani nchini Kenya Raila Odinga ametilia shaka uamuzi wa nchi hiyo kuongoza ujumbe wa kulinda amani nchini Haiti ili kukabiliana na ghasia za magenge huko, akitaja kuwa kama hatua isiyofaa.
Imechapishwa:
Wakati akifanya mahojiano na kituo cha televisheni cha ndani Odinga, alisema kuwa mpango wa kutumwa kwa polisi nchini Haiti haukuwa kipaumbele cha Kenya.
Kiongozi huyo wa upinzani amesisitiza kuwa ukanda wa Afrika Mashariki kwa bado unakabiliwa na kile alichokitaja kama changamoto za kutosha.
Aidha waziri mkuu huyo wa zamani alisema hali ya Haiti ni hatari, akionya kwamba kutumwa kwa polisi nchini humo ni njia moja ya kuhatarisha maisha ya polisi wa Kenya.
Odinga ameeleza kuwa tatizo la Haiti ni la kisiasa na kwamba halihitaji utatuzi wa bunduki pekee bali linahitaji mazungumzo.
Mapema wiki hii, baraza la usalama la Umoja wa Mataifa liliidhinisha kutumwa kwa kikosi hicho kwenda nchini Haiti.
Rais wa Kenya William Ruto katika taarifa yake baada ya uamuzi huo wa UN, alisema ana imani kuwa kikosi hicho kitarejesha usalama nchini Haiti.
Hata hivyo, baadhi ya wakosoaji wamepinga hatua hiyo, wakionyesha shaka juu ya uwezo wa polisi wa Kenya kukabiliana na magenge ya Haiti.