Mgomo nchini Sudan baada ya mazungumzo kukwama
Viongozi wa waandamanaji nchini Sudan, wameitisha mgomo wa siku nzima siku ya Jumatano, baada ya kuvunja kwa mazungumzo na viongozi wa kijeshi.
Imechapishwa:
Siku ya Jumatatu, pande zote mbili zilishindwa kuelewana kuhusu muundo wa serikali ya mpito licha ya kukubaliana kuwa itadumu kwa miaka mitatu.
Jeshi limeendelea kusisitiza kuwa na uwakilishi mkubwa na kuongoza serikali suala, ambalo viongozi wa waandamanaji wanapinga.
Haijafahamika ni lini mazungumzo yatarejelewa tena.
Waandamanaji nchini Sudan wanasema hawataondoka hadi pale viongozi wa kijeshi watakapokubali, raia kutawala serikali.
Mvutano huu unashuhudiwa karibu miezi miwili, baada ya kuondolewa madarakani kwa rais wa zamani Omar Al Bashir, baada ya maandamano ya wananchi, yaliyoanza mwezi Desemba mwaka 2018.