Misri yasitisha ndoto za Cameroon katika michuano ya AFCON
Timu ya taifa ya soka ya Misri imewashinda wenyeji Cameroon mabao 3 kwa 1 kupitia mikwaju ya penalti na kufuzu fainali ya kutafuta kombe la mataifa ya Afrika dhidi ya Senegal siku ya Jumapili.
Imechapishwa:
Mashabiki wa Misri wamesherehekea ushindi wa timu yao ya taifa, baada ya kuwavunja moyo Cameroon katika uwanja wao wa nyumbani wa Olembe jijini Yoaunde, Alhamisi usiku.
Baada ya mechi hiyo ya nusu fainali kuisha kwa timu zote, kutofungana katika muda wa kawaida na ule wa ziada, mikwaju ya penalti ilipigwa kuamua mshindi.
Kipa wa Misri Mohamed Abou Gabal ndiye aliyekuwa shujaa wakati wa upigaji wa penalti, baada ya kuzuia mikwaju miwili kutoka kwa Cameroon, huku mchezaji mwingine Clinton Njie akipiga nje.
Mabingwa hao mara saba wa taji la Afrika sasa watamenyana na Senegal siku ya Jumapili,huku wenyeji Cameroon wakicheza na Burkina Faso siku ya Jumamosi kutafuta mshindi wa tatu.