Brazil yaanza vema michuano ya kombe la dunia 2014, leo ni zamu ya wawakilishi wa Afrika Cameroon
Timu ya taifa ya Brazil hatimaye imeanza vema michuano ya mwaka huu ya kombe la dunia, ikiwa ni nchi mwenyeji wa mashindano ya mwaka huu baada ya kufanikiwa kuchomoza na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Croatia.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Nyota wa mchezo wa hapo jana alikuwa ni kinda anayekipiga na timu ya FC Barcelona ya nchini Uhispania, Neymar ambaye alipachika mabao mawili kati ya matatu yaliyofanikisha kuipa ushindi wa kishindo timu yake.
Waliokuwa wa kwanza kupata bao ni Croatia ambapo mabeki wa Brazil walijichanganya wenyewe na kujikuta wakijifunga wenyewe, bao ambalo lilisababishwa na Marcelo anayecheza kwenye klabu ya Real Madrid ya Uhispania.
B
razil walifanikiwa kusawazisha bao hilo kabla ya kwenda mapumziko kupitia kwa Neymar aliyefunga kwenye dakika ya 29 ya mchezo ambapo timu hizo zikaenda mapumziko zikiwa sare ya bao moja kwa moja.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi ambapo walikuwa ni Brazili waliofanikiwa kupata bao la pili kwa njia ya tuta, bao lililofungwa na Neymar baada ya mchezaji Fred kuangushwa kwenye eneo la hatari.
Adhabu ya Penalty iliyotolewa na mwamuzi raia wa Japan, Yuichi Nishimura ambaye amelalamikiwa na baadhi ya mashabiki kwa kutoa penalty rahisi iliyowawezesha Brazil kupata ushindi mnono.
Bao la tatu la Brazil lilifungwa kwenye dakika ya 90 ya mchezo, likifungwa na mchezaji Oscar ambaye aliwazidi ujanja mabeki wa Croatia walioshindwa kumkimbiza wala kumkaba.
Kabla ya kuanza kwa mtanange huu, kulifanyika sherehe kubwa za ufunguzi wa michuano ya mwaka huu kwenye uwanja wa Sao Paulo uwanja uliokuwa na uwezo wa kupokea mashabiki elfu sitini na tano.
Katika hatua nyingine hii leo wawakilishi wa bara la Afrika timu ya Cameroon itakuwa na kibarua dhidi ya timu ya taifa ya Mexico, huku timu ya taifa ya Uhispania yenyewe ikiwa na kibarua dhidi ya timu ya taifa ya Uholanzi.
Mechi kati ya Uholanzi na Uhispania inakumbusha fainali za kombe la dunia la mwaka 2010 lililofanyika nchini Afrika Kusini na kuzikutanisha timu hizo ambapo Uhispania ilitwaa taji hilo baada ya kuchomoza na ushindi wa bao moja kwa sifuri.