Ufaransa kusaidia kufadhili elimu ya Sayansi kwa wasichana barani Afrika
Wakati Dunia ikiadhimisha siku ya Mwanamke, barani Afrika bado idadi ya wasichana wanaojiunga na elimu ya juu imeendelea kuwa ndogo ukilinganisha na wanaume ambapo ni asilimia 35 pekee ndio wanafanikiwa kujiunga na Vyuo vya elimu ya juu
Imechapishwa: Imehaririwa:
Hayo yamebainika katika Mkutano uliowakutanisha wanawake wabobevu katika sayansi barani Afrika jijini Dar es salaam kujadili mchango wa sayansi katika maendeleo ya wanawake katika kutimiza lengo la usawa wa kijinsia la Umoja wa Mataifa.
Mdhahiri katika Chuo kikuu cha Dar es salaam ambaye pia ni Mkurugenzi wa taasisi ya utafiti wa kisayansi nchini Tanzania Profesa Yunus Mgaya amesema miongoni mwa wasichana hao imebainika kuwa ni asilimia 4 pekee ndio hufaulu na kujiunga na fani za Sayansi ingawaje katika fani za sanaa wasichana wengi wamekua na mwamko.
Naye rais wa Taasisi ya Taaluma ya Sayansi nchini humo TAAS Profesa. Esther Mwaikambo, amesema wasichana kutofanya vizuri katika masomo ya sayansi kumechangiwa na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na utamaduni wa kumkweza mtoto wa kiume na kumkandamiza mtoto wa kike kutokana na mila na desturi za kiafrika
Afisa anayehusika na jinsia wa Shirika la maendeleo la Ufaransa AFD Benardeta Ngwilizi, amesema kutokana na hali hiyo shirika hilo limesaidia kufanikisha miradi ya maji na elimu nchini humo katika jiji la Mwanza ili kuwasaidia wanawake kuondokana na kero za maji na wasichana kupata elimu ili kuinua kiwango cha ufaulu kwa wasichana mashuleni.
Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania Frederic Clavier anasema hatua zitapigwa iwapo usawa wa kijinsia utazingatiwa huku umuhimu wa sayansi kwa watoto wa kike ukiwekewa kipaumbele ikiwa ni pamoja na kushirikiana na taasisi ya taluma ya sayansi ya Ufaransa.
Aidha, Balozi huyo ameahidi kuendelea kushirikiana na serikali ya Tanzania katika kuwawezesha wanawake na kufadhili miradi kuhusu Sayansi, akisema katika dunia ya sasa, ni muhimu Sayansi kupewa kipaumbele katika kutatua matatizo yanayoikabili dunia kwa sasa.
Serikali ya Tanzania imekua ikichukua hatua mbalimbali kuwasaidia wasichana wa kike kufanya vizuri katika elimu Katibu Mkuu Ofisi ya waziri Mkuu sera na Mipango nchini Tanzania Profesa Faustine Kamuzora amesema shule za wasichana zinazofanya vizuri zimekuwa zikikarabatiwa kila mwaka.