Serikali ya Juba yalifungia gazeti la Nation Mirror
Serikali ya Sudan Kusini imelifungia Gazeti la lugha ya Kiingereza la Nation Mirror baada ya kuchapisha taarifa ya rais Salva Kiir na aliyekuwa Makamu wake Riek Machar kuhusu ripoti iliyotolewa wiki hii ikieleza namna walivyojitajirisha baada ya kuanza kwa vita nchini humo mwaka 2013.
Imechapishwa:
Mhariri wa Gazeti hilo Simon Aurelious amethibitisha kufungwa kwa Gazeti hilo kutokana na ripoti hiyo iliyotolewa na Mwigizaji kutoka Marekani George Clooney baada ya kufanya uchunguzi.
Aidha, amesema wameambiwa kulifunga gazeti hilo haraka iwezekanavyo bila ya kupewa taarifa mahususi ni kwanini serikali ya Juba imechukua hatua hiyo.
Siku ya Jumanne na Jumatano wiki hii, Gazeti hilo liliandika kwa kina kuhusu ripoti hiyo iliyomshtumu rais Kiir na Machar pamoja na wakuu wa kijeshi walivyojitajirisha huku maelfu wakipoteza maisha na wengine kusalia wakimbizi.
Hata hivyo, serikali ya Juba imekanusha ripoti hiyo na kuiita ya kipuuzi.
Hii si mara ya kwanza kwa Gazeti hili kufungiwa.
Mwaka uliopita, gazeti hili lilifungiwa kwa miezi tisa baada ya kuchapisha taarifa kuhusu Riek Machar na harakati zake za uasi.