Kenya: Wadau wataka maelezo kutoka kwa mkuu wa polisi
Nairobi – Muungano wa wahifadhi maiti katika hospitali nchini Kenya, umemtaka mkuu wa jeshi la polisi nchini humo, Japhet Koome, kuweka wazi ushahidi kuhusu madai yake kuwa upinzani ulikodisha maiti kuijaribu kuonesha waliuawa na polisi wakati wa maandamano ya upinzani, kauli ambayo imekashifiwa vikali na wadau.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Mkuu wa jeshi la polisi Japheth Koome mapema wiki hii alidai wanasiasa wa upinzani walikodi miili hiyo na kuziweka mahali kulikofanyika maandamano kama njia moja ya kuwalaumu maofisa wake kwa matumizi ya nguvu kupita kiasi dhidi ya waandamanaji.
Licha ya kutoa madai hayo, Koome hakutoa ushahidi wowote kuunga mkono matamshi yake.
Muungano wa wahifadhi maiti katika hospitali umemtaka kiongozi huyo wa polisi kutoa ushahidi au kuomba msamaha kutokana na madai yao ambayo wanasema yanaharibu jina la kazi yao.
Mwezi Julai, shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International katika ripoti yake lilisema kuwa polisi nchini Kenya waliwaua karibia waandamanaji 30 wakati wa maandamano ya upinzani kati ya mwezi Machi na Julai.
Amnesty ilisema baadhi ya vifo hivyo vilitokea baada ya kupigwa risasi na polisi, wengine wakifariki baada ya kushindwa kupumua kutokana na moshi ya gesi za kutoa machozi.
Matamshi hayo ya mkuu wa polisi yamekashifiwa vikali nchini Kenya, upinzani na makundi ya kutetea haki za binadamu wanaotuhumu polisi kwa kutumia nguvu kupita kiasi kuwakabili watu waliokuwa wakiaandamana kwa njia ya amani.
Katika upande mwengine, waziri wa usalama wa ndani Kithure Kindiki na rais William Ruto ambao awali walikuwa wameahidi kumaliza mauaji yanayotekelezwa na polisi, wamewasifia maofisa hao kwa namna walivyowakabili waandamanaji.
Waziri Kindiki aliwasifia polisi kwa kufanya kazi kitaaluma wakati rais Ruto akiwasifia maofisa hao kwa kuhakikisha nchi inautulivu.