Kenya inapoteza Dola Milioni 20 kutokana na maandamano
Nairobi – Chama cha wazalishaji wa bidhaa nchini Kenya, KAM, kinasema taifa hilo la Afrika Mashariki, linapoteza shilling bilioni 2.86 kwa siku kutokana na maandamano yanayoendelea ya upinzani.
Imechapishwa:
Katika taarifa yake, mwenyekiti wa KAM, Rajan Shah, ameeleza kwamba maandamano yanayoendelea yamekuwa pigo kubwa kwa sekta ya uzalishaji, hali ambayo imesababisha hasara kwa biashara ya aina zote nchini humo.
Ripoti ya chama hicho imesema kwamba sekta hiyo inachangia shillingi trilioni moja pesa za kenya katika uchumi wa nchi hiyo kwa mujibu wa utafiti wa kiuchumi wa mwaka huu.
Aidha mwenyekiti huyo ameeleza kwamba maandamno hayo yametatiza hali ya usafiri na usambazaji suala ambalo limekuwa changamoto kwa usafirishaji wa bidhaa katika viwanda.
Licha ya maandamano ya upinzani kutatiza biashara nchini Kenya, KAM inasema huenda maandamano hayo pia yakawaogopesha wawekezaji kuja kufanya biashara nchini Kenya.
Vilevile wametoa wito kwa serikali na upinzani kutafuta suluhu la kumaliza tofauti zao haswa maandamano ambayo yamesababisha uharibifu wa mali na vifo vya raia kuripotiwa.