Kenya: Rais Ruto amewataka wapinzani kutotumia maandamano kufanya fujo
Rais wa Kenya William Ruto, amesisitiza kuwa hana shida ya kuwa na mazungumzo na upinzani lakini akawataka wapinzani wake kuacha kutumia maandamano hayo kufanya fujo, kuharibu mali na kupora.
Imechapishwa:
Matamshi yake ameyatoa wakati huu kinara wa upinzani Raila Odinga, akiapa kuendeleza maandamano hadi pale madai ya raia yatakapotekelezwa na Serikali, huku hivi leo maandamano hayo yakiingia siku ya tatu.
Watu kadhaa wameripotiwa kuawaua katika maandamano hayo wakati wengine mia tatu wakiripotiwa kukamatwa kwa mujibu wa maelezo ya polisi.
Aidha rais Ruto, amewataka polisi kuhakikisha wanawalinda raia na mali zao.
“Kama mko na matatizo kuna njia ya kisheria ya kuendelea, tulikubaliana nao kwamba tufanye mazungumzo ila wameachana na mazungumzo wameenda kujihusisha na vita, siasa yetu haitakuwa ya vita. ” alisema rais Ruto.
Rais wa Kenya William Ruto kuhusu maandamano
Nalo baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki nchini Kenya, limetoa wito wa mazungumzo kati ya rais William Ruto na kiongozi wa upinzani Raila Odinga, ili kumaliza maandamano yanayoshuhudiwa na kutafutia suluhu ya changamoto za kupanda kwa gharama ya maisha.
Aidha, Bara hilo linamtaka rais Ruto kufuta sheria mpya ya fedha kama anavyoeleza Askofu Mkuu Anthony Muheria.
“Gharama ya juu ya maisha imekuwa mzigo kwa Wakenya wengi na imekuwa vigumu kwa família hizo kumudu mahitaji ya kawaida. ” alisema Askofu Mkuu Anthony Muheria.
Askofu Mkuu Anthony Muheria, kuhusu siasa za Kenya
Kiongozi huyo aidha alieleza kwamba wametambua sehemu kubwa ya raia katika taifa hilo wanakabiliwa na ugumu wa kupata mahitaji yao ya kila siku na kwamba kwa sasa sheria hiyo ya fedha ni mzigo mkubwa kwa raia hao ambao tayari wamelemewa na maisha haswa wale wa kiwango cha chini.
Maaskofu hao wametoa wito kwa mkuu wa nchi kuondoa sheria hiyo na kutafuta njia mbadala za kuafikia malengo yanayoendana na hali ya sasa ya uchumi.