Kimbunga kikali Noru chapiga Ufilipino, raia wapatwa na wasiwasi
Kimbunga kikali kiitwacho Noru kimepiga Ufilipino siku ya Jumapili, na kusababisha upepo mkali na mvua kubwa katika kisiwa kikuu cha Luzon. Mafuriko na uharibifu wa mazao vimeripotiwa.
Imechapishwa:
Kimbunga kikali cha Noru kilichoambatana na upepo wa hadi kilomita 195 kwa saa, kimepiga pwani ya kisiwa chenye watu wengi cha Luzon siku ya Jumapili, kama kilomita 80 kutoka Manila, mji mkuu.
Ufilipino hukumbwa na vimbunga takriban mara 20 kwa mwaka, lakini kimbunga cha Noru kimezua wasiwasi kwani kimegeuka haraka kutoka kimbunga hadi kimbunga kikali. Kasi ya pepo zinazoambatana na hali ya hewa iliongezeka kwa kilomita 90 kwa saa katika masaa 24 pekee, kuongezeka "kusiko na kifani", amebaini mtabiri wa hali ya hewa Robb Gile.
Kulingana na mamlaka ya hali ya hewa, kasi ya upepo inaweza kufikia kilomita 205 kwa saa wakati kimbunga kikali cha Nuru, kilichozaliwa katika Bahari ya Pasifiki, kinaelekea katika maeneo mengine ya Ufilipin. Wakati huo huo mamlaka ya hali ya hewa inatahadharisha raia, kwa sababu mafuriko, maporomoko ya ardhi na mawimbi makubwa ya dhoruba yanaweza kuathiri maeneo yaliyoathirika.
Zoezi la kuhamisha raia linaoendelea
Kwa upande wake, mamlaka ya Ufilipino imeanza kuwahamisha wakazi wa miji ya pwani. "Tunawaomba wakazi wa maeneo yaliyo hatarini kutii wito wa kuhama inapobidi," Mkuu wa Polisi wa Ufilipino Jenerali Rodolfo Azurin amesema. Shule zitasalia kufungwa Jumatatu na usafiri wa baharini umesitishwa.
Katika mji mkuu, mvua kubwa na upepo mkali vinatarajiwa, lakini hakuna wakaazi katika vitongoji waliohamishwa Jumapili hii asubuhi. Wakati wa kimbunga kikali cha Raï kilipopiga nchini humo, mnamo 2021, watu kadhaa waliuawa.
Wataalamu wamesema kimbunga hicho kinatarajiwa kudhoofika kitakapo kuwa kikipita kwenye kisiwa cha Luzon, kabla ya kuelekea katika Bahari ya China Kusini siku ya Jumatatu kuelekea Vietnam.