Moto waua watu 41 katika jela lenye msongamano mkubwa nchini Indonesia
Moto uliozuka usiku wa manane katika gereza lenye msongamano mkubwa wa wafungwa huko Jakarta, nchini Indonesia umesababisha vifo vya watu 41 na wengine kadhaa wamejeruhiwa, polisi imesema Jumatano hii Septemba 8.
Imechapishwa:
Moto ulizuka mapema asubuhi Jumatano katika gereza moja huko Tangerang, mji ulio magharibi mwa mji mkuu wa Indonesia.
"Wafungwa arobaini na moja wamefariki dunia, wanane wamejeruhiwa vibaya na 72 wana majeraha madogo," Mkuu wa Polisi wa Jakarta Fadil Imran amewaambia waandishi wa habari.
Picha za televisheni zimeonyesha maafisa wa idara ya Zima moto wakikabiliana na moto ulioteketeza moja ya majengo ya gereza, ukitoa wingu zito la moshi.
Maafisa wa Zima moto wameweza kudhibiti moto huo ambao uliathiri moja ya majengo ya jela hilo, wanakozuiliwa hasa wafungwa waliohukumiwa kwa biashara au utumiaji wa dawa za kulevya.
Mamlaka bado wanachunguza sababu za moto, lakini wengi wamebaini kwamba moto huo ulisababishwa na hitilafu zinazotokana na mifumo duni ya umeme.