Mshtumiwa wa mauaji katika misikiti miwili New Zealand akiri makosa
Raia mmoja wa Australia anayeshtakiwa kwa mauaji ya watu 51 mnamo mwezi Machi 2019 katika misikiti miwili huko Christchurch, nchini New Zealand, ameshangaza wengi leo Alhamisi kwa kukiri mashtaka yote dhidi yake.
Imechapishwa:
Waziri Mkuu Jacinda Ardern na jamii ya Waislamu nchini New Zealand wamefurahishwa na kitendo hicho, na hivyo kuruhusu mahakama kuendelea na kesi hiyo hasa kuchukua uamuzi dhidi ya muuaji.
"Ndio, nina hatia," amesema Brenton Tarrant kutoka gereza la Auckland, kupitia video akihojiwa na Mahakama Kuu ya Christchurch.
Muuaji huyo, mwenye umri wa miaka 29, ambaye alikuwa amevalia nguo za rangi ya kijivu amekiri makosa yanayomkabili bila kushinikizwa na mtu yeyote, chanzo kutoka mahakama Kuu ya ya Christchurch kimebaini.
Brenton Tarrant alikuwa amekana mashtaka 51 ya mauaji, mashitaka 40 ya kujaribu kuua na shtaka moja linalohusiana na kitendo cha kigaidi.
Licha ya kuwa adhabu ya kifo haina nafasi New Zealand, Brenton Tarrant atatumia kifungo cha maisha jela. Mashtaka ya ugaidi na mauaji yanaadhibiwa kwa kifungo cha maisha jela.
Kesi yake, iliyopangwa kudumu wiki sita, imepangwa kuanza Juni 2 huko Christchurch, mji mkubwa kabisa wa Kisiwa cha Kusini, ambapo shambulio dhidi ya misikiti miwili lilitokea Machi 15, 2019.