Nchini Brazil, Lula atuma wanajeshi 3,700 kupambana na uhalifu uliopangwa
Kutokana na hali ya vurugu "mbaya" iliyosababishwa na uhalifu uliopangwa, Rais wa Brazil Luiz Inacio Lula da Silva ameamua kutuma wanajeshi 3,700 katika bandari kuu na viwanja vya ndege vya nchi hiyo hadi mwezi Mei 2024.
Imechapishwa:
"Hali imekuwa mbaya zaidi, vurugu ambazo tumeshuhudia zimezidi kuwa mbaya kila siku." Kutokana na hali hii, Rais wa Brazil Luiz Inacio Lula da Silva ametangaza kutumwa kwa wanajeshi 3,700 katika bandari kuu na viwanja vya ndege vya nchi hiyo.
Jeshi litachukua hatua kwa uratibu na polisi wa shirikisho kuzidisha kukamatwa kwa washukiwa na kuzuia mali za magenge ya wahalifu, hasa huko Rio de Janeiro, kulingana na taarifa ya serikali.
Luiz Inacio Lula da Silva anaona kuwa kuongezeka kwa ghasia kutoka kwa makundi yenye nguvu ya walanguzi wa madawa ya kulevya na wanamgambo wanaojilinda ambao wanadhibiti eneo hilo, hasa mjini Rio de Janeiro, limekuwa suala la usalama wa taifa.
Ameamua kupeleka wanajeshi 3,700 kutoka jeshi la nchi kavu, jeshi la wanamaji na jeshi la anga, katika operesheni inayolenga "kusaidia Brazil kujikomboa kutoka kwa magenge yanayofanya biashara haramu ya madawa ya kulevya na silaha".
"Ikiwa itathibitika kuwa ni muhimu kuimarisha bandari zaidi na viwanja vya ndege, tutafanya hivyo," rais alisema wakati wa mkutano na waandishi wa habari katika Ikulu ya Planalto siku ya Jumatano.
(Pamoja na AFP)