Colombia: Rais Petro azuru China kuimarisha uhusiano wa kiuchumi
Gustavo Petro, rais wa kwanza wa mrengo wa kushoto wa Colombia yuko njiani kwa ziara rasmi ya siku tatu nchini China. Siku ya Jumatano Oktoba 25, atakutana na rais wa China Xi Jinping ambaye alimpokea rais wa Brazil Lula da Silva mwezi Aprili, Nicolas Maduro wa Venezuela mwezi Septemba na Gabriel Boric wa Chile wiki iliyopita.
Imechapishwa:
Ziara hii, kwa mwaliko wa rais Xi Jinping, itafanyika kuanzia Oktoba 24 hadi 26, amesema msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya China, Hua Chunying. Rais Xi Jinping ataandaa sherehe ya kukaribisha na karamu kwa mwenzake wa Colombia. Mao Ning, msemaji mwingine wa wizara hiyo amesema wakuu hao wawili wa nchi watafanya majadiliano ya kuandaa mpango wa maendeleo ya uhusiano kati ya China na Colombia katika enzi mpya, na kwa pamoja watahudhuria hafla ya kutia saini hati za ushirikiano.
Kati ya Gustavo Petro na Xi Jinping, watakuwa na mengi ya kuongea: wawili hao watazungumza kuhusu mpito wa nishati na mapambano dhidi ya umaskini, masuala ya kipaumbele kwa Gustavo Petro. Lakini pia watazungumza juu ya biashara, Barabara za Silk, miundombinu na Mashariki ya Kati, anabainisha mwandishi wetu wa Bogota, Maire-Ève Detoeuf.
Gustavo Petro, ambaye ana ndoto ya kuwa naushirikiano na nchi nyingi, anakusudia kuwafahamisha Wamarekani kwamba Colombia si mshirika tena asiye na masharti kama ilivyokuwa hapo awali, wakati Novemba 3, atakutana na rais wa Marekani Joe Biden.
(Pamoja na AFP)