Malori kadhaa yanayobeba msaada wa kibinadamu yaendelea kuzuiwa kwenye mpaka wa Venezuela
Malori kadhaa yanayosheheni msaada wa chakula na dawa kwa raia wa Venezuela yameendelea kuzuiwa kwenye mpaka wa Colombia na Venezuela.
Imechapishwa:
Utawala wa Nicolas Maduro imekataa msaada huo kuingi nchini Venezuela. Msaada huo ulitolewa na Marekani, Canada, nchi tano za Amerika Kusini na Umoja wa Ulaya. hata hivyo tayari kuna malori mengine ambayo yamewasili katika mji mkuu wa Colombia, Bogota, takitarajia kuelekea kwenye mpaka na Venezuela.
Baadhi ya misaada hiyo itahifadhiwa nchini Brazil, na katika Kisiwa cha Caribbean.
Siku ya Jumatano, Juan Guaido aliyejitangaza rais wa mpito wa Venezuela, alimwomba Rais Maduro kutozuia msaada huo baada ya jeshi kufunga daraja kwenye mpaka kati ya nchi hizo mbili.
Hivi ni vita vipya vinavyozuka nchini Venezuela. Marekani, Canada, na Umoja wa Ulaya wametoa zaidi ya dola milioni 65 kwa ajili ya msaada wa kibinadamu nchini Venezuela. Msaada ambao kwa sasa umewasili nchini Colombia, lakini serikali ya Venezuela imefunga madaraja kadhaa ili kuzuia kuvuka mpaka, anasema mwandishi wetu huko Caracas, Benjamin Delille.
Raia wa Venezuela wanakabiliwa na hali ngumu ya maisha, huku mdororo wa kiuchumi ukiendelea kulikumba taifa hilo.