Shambulio Bogota: Rais Duque atangaza siku 3 za maombolezo ya kitaifa
Shambulio dhidi ya chuo cha polisi katika mji mkuu wa Colombia, Bogota, limeua watu 21 na kujeruhi wengine 68. Shambulio hilo la siku ya Alhamisi ni shambulio baya kuwahi kutokea katika mji mkuu wa Colombia tangu mwaka 2003.
Imechapishwa:
Colombia imeshindwa kuondokana na mchafuko na, vita vya wenyewe kwa wenyewe vimedumu kwa zaidi ya nusu karne sasa.
Rais wa Colombia Ivan Duque ametangaza siku tatu za maombolezo ya kitaifa kufuatia shambulio hilo la bomu lililotegwa katika gari dogo dhidi ya chuo cha polisi nchini, kusini mwa mji mkuu Bogota.
"Idadi ya awali ni watu 21 waliouawa, ikiwa ni pamoja na mshambuliaji, na 68 wamejeruhiwa," Polisi imesema katika taarifa yake, na kuongeza kuwa 58 waliojeruhiwa wameruhusiwa kutoka hospitalini.
Awali serikali ilitangaza kwamba watu 11 waliuawa na 65 walijeruhiwa.
Rais wa Colombia ametaja shambulio hilo kama" kitendo cha kigaidi". Tangu alipochukua hatamu ya uongozi mnamo mwezi Agosti, Ivan Duque ameongeza mapambano dhidi ya kundi la waasi la aELN na biashara ya madawa ya kulevya.
Mshambuliaji amefahamika kwa jina la José Aldemar Rojas Rodriguez, kwa mujibu wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Nestor Humberto Martinez .
Mtu huyu, raia wa Colombia alipoteza maisha katika shambulio hilo, chanzo cha ofisi ya mashitaka kimeliambia shirika la Habari la AFP.