Mamilioni ya Wavenezuela waitikia wito wa upinzani
Wananchi wa Venezuela wamamua kubakia nyumbani, kufuatana na wito uliotolewa na upinzani. Mgomo huu wa saa 24 ni wa kwanza kufanyika nchini humo kwa zaidi ya muongo mmoja.
Imechapishwa:
Katika miji mingine kulishuhudiwa maandamano ambapo waandamanaji walikabiliana na polisi huku polisi ikilazimika kutumia nguvu zaidi kwa kuwatawanya.
Katika makabiliano hayo waandamanaji watatu waliuawa, wengine wengi kujeruhiwa nan baadhi kukamatwa, kwa mujibu wa mashahidi.
Hatua hiyo ni kupinga mipango ya serikali ya kuandika tena katiba mpya, huku rais wa nchi hiyo Nicolas Maduro akikabiliwa na shinikizo la kujiuzulu.
Polisi walitumia mabomu ya kutoa machozi katika miji kadhaa, walipopambana na waandamanaji.
Hata hivyo, katika maeneo yanayounga mkono serikali ya nchi hiyo, hasa katika mji wa Caracas, maisha yaliendelea kama kawaida.
Rais Nicolas Maduro, katika hotuba yake kupitia televisheni, amesema mamia ya wafanyabiashara waliendelea na shughuli zao kama kawaida na kwamba viongozi wa mgomo huo watakamatwa.
Wakati huo huo upinzani umedai kuwa rais Maduro anajaribu kujiimarisha madarakani kwa kubadili katiba, hali ambayo itabadili hali ya sasa ya upinzani kudhibiti bunge.