Donald Trump Junior kuhojiwa na bunge la Senate
Donald Trump Junior, Jared Kushner na Paul Manafort walioshughulikia kampeni ya rais Donald Trump mwaka uliopita, watahojiwa na Maseneta nchini humo wiki ijayo kueleza wanachokifahamu kuhusu madai ya Urusi kuingilia Uchaguzi wa mwaka 2016.
Imechapishwa:
Watatu hao wanatuhumiwa kuwa na mawasiliano ya karibu na serikali ya Urusi kipindi cha kampeni huku, Trump Junior akituhumiwa kukutana na wakili wa serikali ya Urusi.
Inaelezwa kuwa mtoto huyo wa kiume wa rais Trump alikwenda kukutana na wakili huyo ambaye inaaminiwa kuwa alikuwa na habari za kumchafulia jina mpinzani wa baba yake Hillary Clinton.
Wakati uo huo, rais Trump amesema asingemteua Jeff Sessions kuwa Mwanasheria Mkuu ikiwa angeshiriki katika uchunguzi unaoendelea.
Trump amekanusha madai kuwa Urusi iliingilia Uchaguzi na kusisitiza kuwa alikutana na rais Vladimir Putin na kumhakikishia kuwa serikali yake haikuingilia Uchaguzi huo.