Uchunguzi waanzishwa kuhusiana na jaribio la mapinduzi Guinea-Bissau
Serikali ya Guine Bissau imeanzisha uchunguzi kuhusu jaribio la kumpindua Rais Umaro Sissoco Embalo, lililotokea siku ya Jumanne jijini Bissau na kusababisha vifo vya watu 11.
Imechapishwa:
Siku ya Jumanne, watu waliojihami kwa silaha, wamivamia majengo ya serikali jijini Bissau wakati rais Umaro Sissoco Embalo, alipokuwa katika kikao na Mawaziri wake na kuanza kufyatua risasi.
Rais Embalo mwenye umri wa miaka 49, alisema aliponea kuuawa au kujeruhiwa wakati wa makabiliano ya risasi yaliyodumu kwa saa tano kwa lengo la kuindoa serikli yake.
Msemaji wa serikali Fernando Vaz amesema miongoni mwa watu 11 waliouwa ni pamoja na wanajeshi na raia wanne, akiwemo mtumishi wa serikali katika Wizara ya afya pamoja na dereva wake.
Shughuli za kawaida zimeanza kurejea jijini Bissau, wakati huu taarifa za jeshi zikisema uchunguzi umeanza kubaini ukweli kuhusu tukio hili katika nchi hiyo ya watu Milioni Mbili.