Sudan: Maandamano dhidi ya mapinduzi ya kijeshi yaanza kwa amani
Wapinzani wa mapinduzi ya kijeshi wanaandaa maandamano makubwa dhidi ya Jenerali Abdel Fattah al-Burhan, kiongozi mkuu wa mapinduzi yaliyotokea Jumatatu ya wiki hii.
Imechapishwa:
Waandamanaji waameazimia kuanzisha upya mageuzi ya kidemokrasia, licha ya siku tano za ukandamizaji wa umwagaji damu ambao ulisababisha vifo vya watu kadhaa na wengine kadhaa kujeruhiwa. Maandamano ya Jumamosi, Oktoba 20 yameanza mapema alasiri, kwa utulivu.
Tangu asubuhi, waandamanaji wamekuwa wakikusanyika katika maeneo mbalimbali na kwenye barabara kuu kusini mwa uwanja wa ndege. Katika makutano ya barabara kuu mbili mjini Khartoum, waandamanaji wameonekana ni wengi mapema alasiri na wamerudisha tena vizuizi barabarani, ameripoti mwandishi wetu, Eliott Brachet.
Mbele kidogo, kwenye barabara ya uwanja wa ndege, wanajeshi wameweka uzio. Madaraja yanayounganisha Khartoum na miji ya karibu ya Omdurman na Bahri pia yamezuiwa na magari ya kijeshi. Hii ni kuzuia waandamanaji kukusanyika kwenye maeneo ya kunakopatikana majengo ya serikali na jeshi lisielemewe na idadi ya waandamanaji.
Mamia ya maelfu ya watu wanatarajiwa kudai serikali ya kiraia. Haijulikani jeshi litajibu nini. Badala yake, maafisa wa polisi, walitumwa Jumamosi hii asubuhi, kuzuia katika baadhi ya maeneo waandamanaji kujipanga upya.